Habari za leo mpendwa Rafiki msomaji, ni matumaini yangu unaendelea vyema sana na majukumu yako kila siku. Leo katika kipengele cha tabia tunakwenda kuangalia vitu vya Bure vinavyoweza klukufanya uwe mtumwa wa maisha yako yote bila kujielewa. Karibu ujifunze nami.
Kitu chochote unachokipata bila kulipia gharama yeyote au kuweka juhudi hua hakina thamani au wakati mwingine hukipoteza haraka sana. Sasa kuna aina ya bure ambayo huja pale unapokua na tamaa ya kitu Fulani na ikakuletea shida na utumwa katika maisha yako yote. Tuseme leo wewe ni mfanyakazi katika kitengo chochote serikalini au kwenye kampuni yeyote unayofanya kazi halafu una shida ya pesa, au wewe una tamaa ya kufanikiwa haraka bila kutoa jasho.
Mara nyingi kama una tamaa ya kufanikiwa haraka bila kutoa jasho na unawaza kupitia njia rahisi unaweza kukutana na mitego ambayo itakufanya uwe mtumwa maisha yako yote na kamwe usifurahie kile ulichokipata. Tuanze na wanawake umekua unatamani sana nafasi nzuri kazini ambayo utakua juu na husumbuliwi hovyo na mshara mnono, mara ghafla unakutana na bosi mwenye tamaa ya ngono na akatambua shida yako ni nini. Akaweza kukutatulia shida yako kwa kupitia hitaji lake la ngono. Naomba usifikiri kwamba ukishapata kazi au ukishapanda cheo ndio itakua imeishia hapo mtu huyo atakufanya wewe uwe mtumwa wake na atakutumia kila anapokuhitaji. Nimekutana na wengi na najua wengi wanapitia adha hii bila kujua nini cha kufanya. Inawezekana umeolewa lakini kwakua ulikua unataka kazi ukajikuta umetoa mwili wako ili upate kazi au cheo ukua mtumwa maisha yako yote.  Jambo la pekee la kufanya ni kuachana na  hiyo kazi mara moja au kumshitaki mtu huyo mahali panapohusika angalia wewe unachoona kinafaa.
Usikubali kupokea kitu chochote cha bure chenye masharti fulani ili kutimiza shida Fulani inayokutesa sasa hivi unaweza kujikuta mtumwa maisha yako yote. Cha muhimu angalia mtu huyu ana nia gani na hili analotaka nimpe. Wasichana wengi wamekua watumwa wa ngono kwa watu wenye pesa kwasababu tu ya tamaa ya pesa na mitego waliyoingia hawawezi kutoka tena. Acha kutafuta njia rahisi ya mafanikio haipo. Fanya kazi kwa bidi toa jasho upate kile unachokitaka.
Tukija kwa wanaume pia tumekumbwa na utumwa huu kutokana na pale mambo yanapokua magumu sana na unajikuta unatafuta njia rahisi ya kutatua matatizo yako na mwishoe kushia katika utumwa wa milele. Hujawahi kuona viongozi wakifanya mambo ya ajabu ambayo hayaendani na uwezo wao wa kufikiri? Mpaka unajiuliza huyu mtu akili amepeleka wapi! Kumbe alishaingia mtegoni na amekua mtumwa. Tamaa ya fedha rahisi inaweza kukufanya ukawa mtumwa milele. Unaweza kujikuta unapewa cheo ambacho hata hakiendani na elimu yako au uwezo wako ili tu utekeleze matakwa ya mtu aliekuweka pale. Na hili hutokea tu pale anapoona udhaifu wako ulipo mwisho wake unajikuta umekua mtumwa milele na huwezi kutoka au kuacha. Wengi vifo vimewakuta na mambo mengi ya ajabu yasiyofaa kueleza kwa kutamani vitu vya bure au vyeo ambavyo haviendani na uwezo wao kumbe wanakwenda kutumikia matakwa ya waliowaeka.
Kama kuna kitu cha kuogopa sana hapa duniani ni kitu kile kinachokuja au unachokipata na ukakifurahia sana mwanzoni. Jua kwamba huko mbele pachungu sana. Jifunze na kua makini na maamuzi unayoyafanya kila siku maana yaweza kuamua hatma ya maisha yako. Sio kila kinachoonekana kizuri kwa nje ni kizuri ndani. Sio kila kinachokuja na ahadi nyingi nzuri hua ni za kweli. Hivyo tumia ubongo wako sawasawa kufikiri na vilevile kwanza kabisa muombe Mungu wako akuongoze kabla hujafanya maamuzi. Pia tunasema usikilize moyo kama moyo unasita basi tambua huko uendako kuna tatizo.

Rafiki Yako,

Jacob Mushi

Mwandishi na Kocha wa Mafanikio

www.jacobmushi.com/huduma

Andika Maoni Yako Hapa

Discover more from Jacob Mushi

Subscribe now to keep reading and get access to the full archive.

Continue reading