Wakati tunaendelea na Maisha yetu kila siku ni vyema kutenga muda na kujifanyia tathmini ya Maisha yako kwa ujumla na vile vitu unavyofanya kila siku ili ujue upo wapi hasa na unakwenda wapi. Bila kujifania tathmini unaweza kujikuta unatumbukia shimoni na usielewe kinachoendelea. Leo nimekuandalia dalili 7 ambazo zinaonesha wewe huna mpango wa kufanikiwa na hutaweza kufanikiwa kama utaziacha bila kuzitafutia dawa. Mwishoni mwa Makala hii utapata dawa hivyo usiishie njiani kwenye kusoma.

1.Hauna Malengo Unayofanyia Kazi Kila Siku.

Kama wewe huna malengo yeyote kwenye Maisha ambayo unayafanyia kazi kila siku au kila wiki basi hii ni moja ya dalili kwamba hutafanikiwa. Sasa hapa unafanikiwa kwenye nini wakati huna chochote ambacho umekipanga na unakifanyia kazi? Kama unaishi tu kwa kufuata ule utaratibu wa Maisha ambao kila mtu anaufuata utaishia kuwa kama kila mtu. Wenye mafanikio makubwa wana malengo ambayo wanayafanyia kazi kila siku hawasubiri matatizo yaje yawasukume kufanya vitu.

2.Huna Malengo Ya Muda Mrefu.

Kama malengo uliyonayo ni ya muda mfupi tu yaani kuanzia mwaka kushuka chini maana yake huna sehemu yeyote kubwa unayoelekea. Wewe unakuwa ni wale watu ambao wanakusanya hela mwaka mzima halafu ukifika mwisho wa mwaka wanazitumia zote na kuanza upya tena kutafuta. Lazima uwe na malengo makubwa ambayo yanaweza kudumu hata baada ya wewe kuondoka hapa duniani. Waza mbali, tengeneza malengo makubwa kuanzia miaka 50 na kuendelea. Achana na yale maneno kama ipo ipo tu, mwanadamu anapanga Mungu anapangua, hizo ni dalili za kuwa maskini Maisha yako yote. Wewe Maisha yako unachowaza ni kula, kulala, kuvaa na kuwa na familia basi, ndugu yangu ongeza Zaidi ya hapo.

3.Hauna Tabia ya Kuweka Akiba.

Ndio kama huna tabia ya kuweka akiba maana yake huwezi kufikia mafanikio makubwa, bila kujalisha unapata kiasi kidogo vipi weka akiba. Akiba itakusaidia kutimiza yale malengo makubwa ambayo yanahitaji pesa nyingi. Hakuna mahali unaweza kupata pesa za muujiza ukatimiza yale malengo makubwa uliyonayo. Anza kujiwekea akiba sasa uondokane na dalili hii ya kutokufanikiwa kabisa. Usiwe mtu anaesema siku nikipata hela nitafanya hiki na kile wakati unajua siku zote huwa unapata hela lakini wazitumia zote. Unajua ukiweka elfu moja kila siku kwa mwaka mzima utakuwa na tsh 365,000/= (laki tatu na sitini na tano) hii pesa ungeweza kununulia lile shamba ulisema ukipata utaenda kununua au yale malengo ambayo uliyonayo. Hakuna mahali pengine utapata pesa kama hujiwekei akiba.

4.Unalalamika na Kulaumu Wengine.

Kama una tabia za kulalamika na kulaumu wengine kwasababu yeyote ile hiyo nayo ni dalili za kutokufanikiwa kabisa Maishani mwako. Tabia kuu ya waliofanikiwa ni Kuchukua hatua na sio kulalamika na kama jambo hawana uwezo wa kulibadilisha basi wanaachana nalo kwasababu kulalamika hakubadili chochote. Mungu mwenyewe hapendi watu wanaolalamika na kulaumu sasa wewe unategemea kweli utafanikiwa kama una tabia hiyo?

5.Huamini Kwamba Mafanikio Ni Mchakato.

Wewe bado una mawazo yale ya “ipo siku nitafanikiwa” halafu hakuna cha maana unachokifanya ili hiyo siku ya kufanikiwa itokee. Rafiki hii pia ni dalili ya kutofanikiwa kabisa. Hakuna siku ambayo itatokea ghafla halafu ukajikuta tayari umefanikiwa. Lazima uwepo mchakato ambao unakupeleka kwenye mafanikio makubwa kidogo kidogo. Achana na hayo mawazo ya ipo siku halafu hakuna unachokifanya, hapo unasubiria embe chini ya mti usio na matunda yoyote.

6.Mwaka Umeanza na Mpaka Sasa Hujajifunza Kitu Chochote Kipya.

Kama mpaka unaposoma Makala hii hujaweza kununua kitabu chochote, hujaweza kusoma kitabu chochote ambacho hukuwahi kukisoma, hujadhuria semina yeyote iwe mtandaoni au ana kwa ana basi Rafiki una dalili ya kutokufanikiwa. Kujifunza ni mojawapo ya tabia za watu waliofanikiwa sana sasa kama wewe bado hujaweka mpango wowote basi unaelekea pabaya. Lakini usiogope mwishoni mwa Makala hii kuna habari njema kwa ajili yako.

7.Huna Ratiba Yaani Unaishi kwa Kufuata Matukio.

Hapa yaani wewe ni mtu ambaye unasubiria matukio ndio yakupangie nini cha kufanya. Huna mipango yako binafsi mpaka usikie Rafiki zako wanasemaje au wanataka kwenda wapi wewe ndio uende. Unaamka asubuhi kwenda kazini kila siku lakini hujawahi kuwa na mipango yako binafsi yaani kama hakuna kazi basi wewe huna cha kufanya. Rafiki hii pia ni dalili, kama unasubiria mipango ya wengine ndio mipango yako ikae sawa hapo pana shida. Lazima wewe binafsi uwe na tabia ya kujitengenezea ratiba zako mwenyewe. Usisubirie mipango ya wengine.

Nyongeza.

Unashinda Baa Kila wikiendi.

Yaani kama na wewe kila wikiendi lazima uende ukastarehe wengine wanasema kula bata, hiyo nayo ni dalili ya kutokufikia mafanikio makubwa. Hii ni kwasababu watu wengi wanaoishinda baa Zaidi wanaenda kutumia na sio kutengeneza pesa. Usijindanganye unakwenda kubadilishana mawazo baa, hayo mawazo ya aina gani yanayosisimuliwa na vilevi? Hayo ni mawazo yenye maana kweli? Mawazo yanapatikana sehemu yenye utulivu na sio baa kwenye kila aina ya kelele na uchafu. Wewe endelea na tabia za aina hii halafu utakuja kusema hujui pesa zinapokwenda.

HABARI NJEMA;

Kama wewe Rafiki una dalili hizi, na umeweza kuisoma Makala hii napenda kukushirikisha dawa ambayo itakusaidia. Ni msaada wa karibu kutoka kwangu ambao utakusaidia kwa mwaka huu mzima, unapata nafasi ya kuongozwa kwa mwaka mzima kwenye malengo yako na zile tabia ambazo zimekuwa zinakukwamisha nakusaidia uweze kuziacha kwa kukusimamia bonyeza hapa www.jacobmushi.com/coach

Jiunge na Mtandao wetu uwe unapokea makala hizi moja kwa moja kwenye email yako. Mwishoni mwa makala hii kuna sehemu ya kuweka email na chini yake pameandikwa Subsrcibe. Weka email kisha Bonyeza Subscribe.

Ubarikiwe sana,

Rafiki Yako, Jacob Mushi

www.jacobmushi.com/coach

4 Responses

Leave a Reply to AgustineCancel reply

Discover more from Jacob Mushi

Subscribe now to keep reading and get access to the full archive.

Continue reading