Katika Maisha yetu tunapitia hali za aina mbalimbali kutokana na aina za watu tunaoishi nao. Mara nyingi hasa kwenye kipindi hiki kumekuwa na uongo uliopitiliza katika biashara, mahusiano na hata kazi zetu kwa ujumla.
Ubaya wa uongo huu ni kwamba ili uweze kudanganya vizuri inakupasa uwe na kumbukumbu ya kile ulichokidanganya mara ya mwisho. Wakati mwingine tunajisahau kwamba tulishadanganya tena hivyo uongo wetu kuonekana Dhahiri.
Naomba utambue mwisho wa uongo ni ukweli kujionyesha hadharani haijalishi umedanganya mara ngapi au unaendelea kudanganya ipo siku utaaibika. Ukweli pekee ndio unakupa uhuru. Uhuru wa nafsi yako mwenyewe. Uhuru wa kufikiri.
Uongo unakuleta utumwa maana itakubidi uwe unajiandaa kila wakati kujibu juu ya uongo uliousema. Uongo unakufanya uishi kwa wasiwasi kana kwamba unadaiwa. Uongo ni deni. Ukidanganya lazima uje ulipie deni la uongo wako.
Kwa namna yeyote ile njia ya mwongo ina mwisho wake. Kuna siku atashindwa kudanganya na itaonekana kwamba huwa anadanganyaga kila siku.
Mojawapo ya kitu kikuu kinachovunja mahusiano ya aina zote unazojua ni uongo. Hata majambazi waliokwenda kuiba sehemu huwa wanagombana pale mmoja wao anapoingia tamaa na kudanganya wenzao ili anufaike Zaidi.
Ni hatari sana uongo unapokuwa tabia yako kwani ni ngumu sana kuicha. Uongo ukiwa tabia yako utakutesa sana maishani mwako. Hata mwongo mwenyewe hapendi kudanganywa.
Hakikisha unakuwa mkweli kwenye njia zako hutahitaji kuwa na kigugumizi unaoulizwa maswali.
Tukitaka kuwa na mafanikio  ya kweli kwenye Maisha yetu tuache kudanganya. Ili tuweze kufurahia Maisha tuache kudanganya. Haimaanishi tuseme kila kitu ila tuwe na kiasi katika kusema kwetu lakini tusidanganye.
Karibu sana.
Jacob Mushi.

Andika Maoni Yako Hapa

Discover more from Jacob Mushi

Subscribe now to keep reading and get access to the full archive.

Continue reading