Kama hadi sasa unaamini kwamba waliofanikiwa wana bahati hivyo wewe una bahati mbaya, sahau kabisa kuhusu kufanikiwa. Kwa kusema hivyo tayari umejiwekea vikwazo wewe mwenyewe vya kusonga mbele. Badilisha mtazamo wako ili uweze kusonga mbele.
Kama bado hadi sasa una amini katika bahati nasibu au ukutane na dili Fulani likutoe utaendelea kusubiri sana ndugu yangu. Hakuna dili au bahati ya kukutoa Zaidi ya hii kufanya kile unachokipenda tena ukifanye kwa nguvu zote na kwa bidii.
Kama bado na wewe una Imani kwamba watu wenye mafanikio yaani matajiri ni wachawi au wameiba, au mali zao sio halali endelea kuamini hivyo uone kama utakuja kumiliki mali hata siku moja. Achana na Imani potofu juu ya watu wenye mafanikio. Kama kweli unataka utoke sehemu hiyo uliyopo anza kuwapenda wale waliofanikiwa. Haiwezekani hata siku moja wewe ukawa kile kitu unachokichukia. Utakuwa kile unachokipenda. Kama unapenda kuwa maskini utabakia maskini.

Siko zote akili ya mwanadamu inaposhindwa kujishughulisha hivyo hutafuta sababu rahisi ambayo itamfanya aendelee kubaki vile alivyo. Hatari kubwa inakuja hapo ni kwamba hauwezi tena kubadilika kwasababu kitendo cha kusema matajri ni wachawi na washirikina maana yake huwezi kuwa tajiri wewe. Kwasababu ukisema uwe tajiri umeachagua kuwa mshirikina na mchawi. Kitu cha ajabu ni kwamba ukimwambia mtu huyu anaesema matajiri ni wachawi atoe uthibitisho hana cha maana cha kukuambia. Zaidi ataanza kukueleza hadithi alizozisikia kwa watu.

Ndugu yangu hauwezi kufanikiwa nje ya kile unachokiamini hata siku moja. Kama unaamini Kufanikiwa ni kufanya kazi kwa bidii basi bidii ndio itakuletea mafanikio. Badilisha Imani zako ulizonazo na maisha yako yatakwenda kubadilika. Hakuna kazi ngumu kama kubadilisha imani ya mtu.

Akili ya mwanadamu usipoilazimisha kujishughulisha hua inalala. Kama hutajilazimisha kufanya mambo hata wakati umejisikia kuchoka au kuzoea hali uliyonayo huwezi kupata mabadiliko. Kila kitu kinawezekana kama ukiamini inawezekana.
Unatamani kuwa maskini kwasababu maskini wapo wengi hivyo hutabakia mwenyewe. Ila ukweli ni kwamba hakuna kitu kizuri ambacho kila mtu anacho. Ukiona kitu kila mtu anaweza kuwa nacho basi hicho kitu thamani yake ni ndogo. Usikubali kuwa kama wengine tumia uwezo mkuu uliopo ndani yako ili ufikie mafanikio.
Kitu cha muhimu kufanya ni kuibadilisha Imani yako juu ya watu waliofanikiwa na juu ya mafanikio yenyewe. Mafanikio sio bahati, sio kuzaliwa kwenye familia ya kitajiri, sio kuwa na watu mashuhuri wanaokujua, ni kufanya kazi kwa bidi juu ya kile ulichokichagua kukifanyia kazi, kujifunza kila siku, kujichanganya na waliofanikiwa au wenye mawazo na vitendo vya mafanikio. Acha fikra potofu waza chanya kwenye kila jambo unalokutana nalo utafikia  ndoto yako.
Your Partner in Success
Jacob Mushi
Entrepreneur & Author

Andika Maoni Yako Hapa

Discover more from Jacob Mushi

Subscribe now to keep reading and get access to the full archive.

Continue reading