Ushawahi kuona mtu amefanya jambo kwa kujiamini sana sasa katika kujiamini kwake kupita kiasi akajikuta haoni hata makossa yake. Inapotokea watu ambao wanamtazama wakamwambia kwamba hapo unakosea, usifanye hivyo fanya hivi. Yeye anaanza kuchukia na kuona kwamba ameonewa, au wale watu wanaomwelekeza wanamwonea wivu.

Ukitaka kusonga mbele na kukua Rafiki yangu lazima uweze kutofautisha kati ya kukosolewa kwa uzuri na kukatishwa tamaa. Kuna watu wamekuzidi umri, wengine wamekuzidi maarifa, wengine walishapita huko ulipo sasa hivi. Wakikwambia ukweli kuhusu mwenendo wako kubali kusikia na kuelewa pale ulipoelekezwa.

Huwezi kufanikiwa hata siku moja kama hutakuwa na tabia ya kunyenyekea pale unapoonywa. Kama ukiambiwa ukweli wewe unanuna basi ujue hujakua kiakili kwenye kile unachokifanya. Lazima uweze kujua huyu mtu ananikosoa kwa uzuri na sio kunikatisha tamaa.

Mtu ambaye anakukatisha tamaa mara zote atakwambia tu huwezi au katika kukukosoa kwake hakuelezi ni kitu gani hasa unapaswa kufanya ili kurekebisha pale alipoona unafanya vibaya. Watu wa aina hii ndio unatakiwa uwaelewe kama wakatishaji tamaa. Hawa wanakuwa na mifano mingi ya waliofeli sana na hawana mfano hata mmoja wa waliofanikiwa. Hawataki kukupa suluhu la tatizo kwasababu lengo lao ni uache na sio usonge mbele.

Ukiweza kuelewa tofauti hii ya wakatishaji tamaa na wanaokukosoa kwa uzuri kwa ajili ya kukupa changamoto utafanikiwa kwenye kile unachokifanya. Usiwe mtu wa kukata tamaa pale unapoambiwa ukweli. Kuwa mwelewa na usonge mbele.

Ni mimi Rafiki Yako, Jacob Mushi
#UsiishieNjiani
“Piga Hatua, Timiza Ndoto Yako.”
Jipatie Vitabu vya Biashara na Mafanikio… https://jacobmushi.com/patavitabu

Andika Maoni Yako Hapa

Discover more from Jacob Mushi

Subscribe now to keep reading and get access to the full archive.

Continue reading