Habari rafiki, leo nataka nikuonyeshe njia mbalimbali za kupata wazo la biashara na mtaji. Inawezekana mwaka huu una mpango wa kwenda kuanza biashara yako mpya Makala hii itakua msaada kwako. Inawezekana pia una wazo la biashara lakini hujui utatoa wapi mtaji Makala hii pia itakwenda kukuonyesha mwanga.

Njia za kupata WAZO LA BIASHARA:

Ni kitu gani kinaongeza thamani kwenye Maisha ya wengine? Ni kitu gani ukikifanya hapo ulipo utafanya watu wafurahie Maisha yao? Ni kitu gani kitafanya Maisha ya watu unaowafahamu yawe marahisi? Ukiweza kujua vitu hivyo hapo utakuwa umepata wazo la biashara na unaweza kuanza na kufikia mafanikio makubwa sana. Kama unataka wazo lako lidumu hakikisha unachagua kitu ambacho watu wataendelea kukihitaji kwa muda mrefu sana. Mfano labda ni vocha zinapatikana kwa shida ukiamua kuwapelekea vocha hakuna siku shida yao ya vocha itakwisha. Lakini ukiwauzia masweta ya kupunguza baridi ujue kuna kipindi cha joto hawatahitaji masweta au wanaweza wakatunza masweta yao mwisho wateja wakapungua. Mtu aliegundua internet na anaemiliki mitandao ya simu hawa ni watu ambao biashara zao zitadumu kwa muda mrefu sana duniani hadi pale mapinduzi mengine ya teknolojia yatakapokuja. Embu jiulize ni tatizo gani la kujirudia rudia lipo kwenye jamii yako ulete suluhisho Maisha ya wetu yawe bora.

SOMA: JINSI YA KUZISHINDA CHANGAMOTO KWENYE BIASHARA NA UJASIRIAMALI

Kwenye matatizo kuna aina mbalimbali ya matatizo kwenye jamii. Unaweza kuangalia ni tatizo gani kubwa linaikumba jamii yako ukatafuta suluhisho na ikawa ni biashara yako kubwa sana. Kamwe hata siku moja usiweke faida mbele kwenye kutatua matatizo ya watu. Wateja wako watakukimbia. Ndio unahitaji faida sana lakini ongeza bidii Zaidi kwenye utatuzi wa tatizo. Wengi wetu hujisahau mwanzoni unaanza vizuri ukishapata pesa kidogo unaanza kusahau kama upo pale kutatua matatizo ya watu. Watu wana matatizo mengi sana kwenye jamii zetu angalia ni aina gani ya tatizo unaloweza kuliletea suluhisho kisha ulikuze iwe ni biashara yako.

Una kipaji? Unapendelea kufanya kitu Fulani Zaidi? Je unajua kwamba unaweza kugeuza kipaji chako au unachopenda kuwa wazo la biashara? Mfano unapenda kuchora, unaweza kuchora kwa biashara. Unaweza kuwachora watu ukawapa wakakulipa. Unapenda kutunga hadithi? Unaweza kuandika hadithi zako ukaziuza ua ukaziweka mtandaoni watu wakasoma baada ya muda ukaweka gharama ya kulipia ili wasome hadithi zako. Au ukaandaa vitabu vya hadithi zako ukauza. Karibu kila ulichonacho unaweza kukigeuza kuwa wazo la biashara. Kasoro kuuza mwili wako au kulala. Kama bado hujajua una kipaji gani au unachokipenda utakigeuzaje kuwa wazo la biashara wasiliana nami kwa ushauri Zaidi.

SOMA: KAMA UNASIFA HIZI WEWE NI MJASIRIAMALI

Una ujuzi wowote au uzoefu katika jambo Fulani? Unaweza kutumia hiyo kama wazo lako la biashara na ukajiajiri. Tuchukulie mfano wewe umesomea IT (Information Technology) halafu unaweza Zaidi kutengeneza Website au kutengeneza matangazo ya picha. Hilo tu linatosha wewe kuanza kama biashara yako na ukaikuza taratibu hadi ikafikia kuwa biashara kubwa sana. Tatizo la wengi hawataki kupata hasara, hawataki kuanzia chini, hawataki kufanya kazi kwa bidii na ubunifu. Mtu anataka aanze leo halafu kesho apate idadi ya wateja anaowataka. Hiyo haiwezekani kirahisi hivyo labda utumie jina la mtu. Kubali kuumia, vumilia na mwisho wake utaona matunda ya jasho lako.

Watu wanahitaji nini kwenye jamii yako? Kwa mfano ukiona watu wengi wanakimbilia kwenye kilimo badala na wewe kukimbilia kulima unaweza kuwauzia mbegu, au ukawapa elimu bora juu ya kilimo wanacholima. Inawezekana unafahamu vitu vingi sana kichwani kwako na watu wanavihitaji hadi sasa hujajua kama unaweza kutumia hiyo kama biashara yako? Jaribu kuitazama jjamii uliyonayo kisha utagundua inahitaji nini na wewe una kitu gani ambacho unaweza kuipatia. Hivi sasa tuna vijana wengi ambao wamemaliza chuo na hawana ajira. Kitu cha kushangaza sana ni pale mtu anaposhindwa kuwaza ataitumiaje elimu aliyoinayo atengeneze kipato. Kama uliweza kwenda kusomea kitu chuoni miaka 3 halafu leo unakaa nyumbani mwaka mzima huna cha kufanya huoni ulikuwa unapoteza muda?  Jaribu leo kutafakari unawezaje kuutumia ujuzi au elimu uliyonayo kujiajiri au kama wazo la biashara. Kama bosi wako angekutumia wewe ili akulipe kwanini unashindwa kufikiri ni kwa namna gani ujitumie ujilipe?

Ni mimi Rafiki Yako,

Jacob Mushi

USIISHIE NJIANI

Piga Hatua, Timiza Ndoto Yako.

Andika Maoni Yako Hapa

Discover more from Jacob Mushi

Subscribe now to keep reading and get access to the full archive.

Continue reading