Ni kweli hutakiwi kufanya kutafuta maadui kwasababu haina maana yeyote, ila katika safari ya mafanikio huwezi kuepuka kuwa na maadui. Kuna watu watakuchukia tu bila sababu yeyote. Wengine watakuchukia kwasababu kile unachokifanya wao hawajaweza kufanya, wengine watakuchukia kwasababu wameona umeanza kuwapita kwasababu mnafanya kitu kinachofanana.

Sasa wakati mwingine ili kujua kama kweli unasonga mbele na unafanya mambo ya tofauti ni pale unapokutana na watu ambao wanakuchukia. Inakupasa uelewe kwamba maadui hawaji kwako sio kwasababu unafanya kitu kibaya bali ni kwasababu unafanya kitu kizuri sana hadi unawakera.

Kuna wakati naanza kuandika walitokea watu wakaanza kuniambia wewe unaandika sana hadi unakera, unapost sana Makala zako. Nikagundua Kumbe nimefanya hadi wameanza kuona.

Unachotakiwa kujua maadui wanapokusema wanakutangaza, watu wanaposema mambo yako wanawaambia watu ambao walikuwa hawakujui kwamba kuna jamaa anafanya jambo Fulani la tofauti. Sasa mojawapo ya kipimo cha ukubwa wako sio watu wengi wanakusifia tu bali hata wale ambao wanakuchukia bila ya sababu.

Unachotakiwa kujua kwamba:

Huwezi kumfurahisha kila mtu.

Unapokuwa tofauti na wengi ndio maadui watakuja wengi.

Maadui wanapokusema wanakutangaza kwa wale ambao hawajasikia Habari zako tena bure.

Endelea mbele, fanya kazi zako kwa ubora na maadui watakuja wenyewe. Hutakiwi kutengeneza maadui hata mara moja wewe unatakiwa kuwa bora tu na wa tofauti katika kile unachokifanya. Usipoteze muda wako kujibizana nao wewe endelea na kazi matokeo ya kile unachokifanya ndio yatatoa majibu.

Nikusihi Rafiki kama huna adui maana yake wewe bado hujawa tishio kwa mtu yeyote hapa duniani. Hivyo basi nenda kafanye jambo la tofauti na la kipekee ambalo litawashtua wale waliokuwa wamelala waanze kuzungumza Habari zako.

Nenda kafanye jambo la tofauti sana na la kipekee uwapatie kazi wengine, hivi unajua kuna watu hawana cha kufanya sasa kama ukianza kufanya kwa ubora unakuwa unawapa cha kufanya. Unawapa kazi ya kukusema, unawapa kazi ya kukufuatilia, unawapa kazi ya kuandika mabaya yako.

Ubarikiwe sana,

Rafiki Yako, Jacob Mushi

Andika Maoni Yako Hapa

Discover more from Jacob Mushi

Subscribe now to keep reading and get access to the full archive.

Continue reading