Unapokuja na sababu ya kwamba kinachokuzuia ni kukosa mtaji unakuwa umeizuia akili yako haki yake ya msingi kabisa ya kufikiri. Kwenye mazingira uliyopo kama una watu kumi tu wanaokujua na wewe unawajua hao wangetosha kuwa wateja wako wa kwanza kwenye biashara yako mpya.

Moja; Kama watu hao kumi kuna kitu cha aina moja wanatumia labda tuseme wote wanakunywa chai ya kununua. Kama wewe una elfu kumi hua unaipata na unaona ni ndogo unaweza kuanza nayo kwa biashara ya chai. Waambie hao watu kumi wanaokujua wasiende tena kununua chai kule walipozoea wewe utakuwa unawaandalia na kuwaletea majumbani mwao.

Hapo tayari utakuwa umeanza biashara yako. wakiipenda chai yako na huduma yako waambie wakawaambie marafiki zao watatu kila mmoja. Marafiki zao wakikubali tayari utakuwa na wateja 40 jumla. Kama wateja hawa watakuwa wanakunywa wote chai asubuhi na unatengeneza faida ya tsh mia kwa kila kikombe wewe unakuwa umeweka sh elfu nne asubuhi mfukoni kabla hata wengine hawajaanza kujua wafanye nini leo.

Kwasababu mpaka sasa hivi huna mtaji lakini unapata pesa ya matumizi mengine ya muhimu ndio maana upo hai hujafa njaa basi faida utakayopata kwa mwezi mzima usiitumie irudishe kwenye biashara yako.

KUMBUKA HAPA SIO LAZIMA IWE CHAI,angalia mwenyewe ni kitu gani hawa watu kumi wanakifanya kwa pamoja na huwa wanalipa pesa ili kukipata. Kama wewe unaweza kuwafanyia na kitu hicho unaweza kukianza kwa bei nafuu kianze.

Mbili; Kama una marafiki zako watano wenye magari na wewe huna gari, huna biashara yeyote. Hawa marafiki zako huwa wanakwenda kuosha magari yao. Embu waambie wasiende kuosha tena hayo magari kule car wash bali wewe utakuwa unawaonshea majumbani mwao kwa gharama nafuu. Kwasababu hawa ni marafiki zako. Hawapendi waone unakaa bila ya kazi pasipo na shaka watakupa wewe hiyo kazi. Kwasababu hawapendi uje uwasumbue kila siku huna hela watakupa hiyo kazi.

Hawa marafiki zako wana marafiki zao wenye magari embu waombe wakusaidia kuwaambia kwamba kuna rafiki yao mmoja anatoa huduma ya kuosha magari nyumbani. Kwasababu wanaaminiana watasema uende ukawaoshee na wao. Kumbuka hapa mtaji wako ni ndoo, sabuni na dodoki la kusugulia gari. Wale marafiki zako watano wakiwaambia marafiki zao kila mmoja wawili wawili utakuwa na wateja wapya 15. Sasa piga hesabu hawa marafiki wakiosha magari yao kila baada ya siku tatu au nne utakuwa unatengeneza shilingi ngapi?

KUMBUKA HAPA SIO LAZIMA IWE GARI ANGALIA MARAFIKI ZAKO WANA VITU GANI VINGINE WANAVYOKWENDA KULIPIA ILI WAHUDUMIWE. KAMA UTAWEZA WEWE KUWAHUDUMIA NA UKAANZA KWA GHARAMA NDOGO NENDA KAFANYE.

Tatu; Una kitu gani unakijua na unafikiri watu wengi hawakijui na ukiwafundisha kinaweza kuwasaidia kwenye kazi zao? Mfano wewe unajua kutumia mitandao ya kijamii. Kwanini usiwafate wafanyabiashara hasa wale wanaokujua kwanza waelezee nguvu ya mitandao hii. Waambie jinsi ina watu wengi. Waaambie unaweza kuwafungulia kurasa za biashara zao na ukawafundisha jinsi ya kutumia na  wakakulipa pesa kidogo. Embu wafungulie ukurasa wa Instagram na Facebook waelekeze jinsi ya kutumia kisha watoze tsh elfu kumi tu.

Waambie wakuonyeshe marafiki zao wengine ambao wanahitaji huduma kama hiyo. Ukiweza kuwahudumia watu kama hamsini hivi ndani ya mwezi mzima una laki tano za Kitanzania na tayari umeweza kuanza biashara nyingine kubwa tu.

Kwanini nimependa kutumia marafiki, watu wanaokujua, na unaofahamiana nao. Hii ni kwasababu kubwa kwamba unapoanza biashara mpya au kitu kipya watu ambao ni rahisi kukubaliana nacho ni wale wanaokujua. Hawa watu sio rahisi wakufukuze waseme leo sina hela njoo siku nyingine. Hawa watu watakubali bidhaa zako kwasababu wanaona wanakusaidia.

Hivyo basi kuepuka changamoto za kukatishwa tamaa na kurudishwa nyuma, kufukuzwa na wakati mwingine kuambiwa maneno makali anza na hawa marafiki zako, au watu wanaokufahamu.

Sidhani kama kuna mtu mwenye akili timamu atakukatisha tamaa na anapenda maendeleo yako. Sidhani kama kuna mtu rafiki yako kweli anapenda uje umwombe pesa kila siku. Vile vile hawa watu kwa mara ya kwanza hawataweza kukukopa kwasababu wanaona kile unachokifanya sio kitu kirahisi.

Usikubali kulalamikia mazingira. Kama mazingira unayoishi kuna binadamu basi kuna fursa ya kutengeneza pesa kila siku.

USIIPE AKILI YAKO UKOMO WA KUFKIRI. ENDELEA KUFIKIRI UTAONA UMEZUNGUKWA NA FURSA NYINGI SANA.

Jacob Mushi

USIISHIE NJIANI

“Piga Hatua”

Andika Maoni Yako Hapa

Discover more from Jacob Mushi

Subscribe now to keep reading and get access to the full archive.

Continue reading