Siku moja nilikutana na kijana mmoja anaitwa Baraka ambaye alikuwa na changamoto ya kukatiwa tamaa yaani kuchokwa na watu wa karibu yake kama wazazi, mpenzi wake na kadhalika. Baraka alinieleza kuwa ilifika mahali akasema sasa afanye nini tena maana kila anachokifanya wale waliomkatia tamaa wanakuwa wanaendelea kumkatisha tamaa.

Ilifika mahali akiwaeleza wazo lolote jipya ambalo ameona litafaa kufanya mfano kama wazo la biashara Rafiki zake na ndugu zake walimcheka na kumwambia; “wewe tumeshakuzoea kila siku unakuja na hadithi zako za kufanikiwa tu lakini hatuoni matokeo yeyote. Embu badilika kwanza ndio utueleze kitu tukuelewe.”

Hali hii ilimkatisha tamaa sana hasa pale alipokuwa anataka kujaribu kitu kwasababu akikumbuka Maneno hayo mabaya anaishiwa nguvu. Akili yake inamwambia atakataliwa tena.

Ilifikia kipindi mahusiano yake na mpenzi wake yakawa mabovu sana. Hii ni kwasababu walikuwa wanagombana kila siku na mpenzi wake. Msichana yule ambaye alikuwa anapenda starehe alikuwa hamuelewi kabisa alipoelezwa kuwa hakuna pesa kwa sasa.

Baraka ananiambia ikafika mahali ilibidi asitishe mahusiano yake na binti yule. Japokuwa alikuwa anampenda sana lakini hakuwa na namna ya kuendelea nae kwasababu alikuwa kama kidonda. Rafiki zake waliokuwa wanamsema vibaya na kupinga kila alichokuwa anawaambia aliamua kuacha kabisa kuwaeleza chochote.

Walibakia ndugu zake wa karibu haswa baba yake ambaye mar azote ndio huenda kumuomba fedha kwa ajili ya mtaji wa biashara aliyokuwa anaifanya. Halafu sijakwambia kwamba Baraka alifeli shule kidato cha nne hivyo yeye pekee ndie aliebakia nyumbani akifanya shughuli za biashara. Baba yake alimwambia nimechoka kukupa pesa kila siku za mtaji halafu sioni maendeleo yeyote. Kila siku unakuja na wazo jipya la biashara lakini hakuna unalofanikisha hata moja.

Baba alifikia kumwambia kuwa amemchoka. Akamwambia atafute njia nyingine au kitu kingine cha kufanya kinachoeleweka. Baraka alisema alifikia mahali akaona kabisa amekata tamaa ya Ndoto yake kubwa ya kuwa Mjasiriamali mwenye mafanikio. Aliona zile hadithi za matajiri walianzia chini sijui waliuza viazi, wengine wanasemaga waliuza genge akaanza kuziona ni za uongo.

Baraka alipofika hapo nikamwambia asiendelee kusema tena. Nikamwambia neno moja kwamba “WENGINE WANAPOKUKATIA TAMAA, KUMBUKA MUNGU BADO HAJAKATA TAMAA NA WEWE NA NDIO MAANA BADO UPO HAI UNAPUMUA NA NI MZIMA”. Wengine wanapokukatia tamaa wewe mwenyewe usikubali kuungana nao na kukata tamaa pia.

Wengine wanaposema wamekuchoka wewe usikubaliane nao kwasababu hawajui kile ambacho umekibeba ndani yako. Wengine wanaposema mawazo yako sio halisi na hayawezekani waambie waendelee kusubiri.

Hakuna aliefanikiwa bila ya kukataliwa, kuna wakati unakataliwa na watu ili uweze kupata watu wengine bora Zaidi. Kuna nyakati Mungu anafanya watu wale ambao wangeweza kukusaidia wasikusaidia ili uweze kuona ukuu wake.

Usikubali kukata tamaa pale wengine wanapokata tamaa juu yako. Kumbuka Mungu hajakata tamaa na wewe. Hilo ndio jambo pekee la kukutia nguvu. Hii ndio hamasa ya kwanza ya wewe kusonga mbele Zaidi.

Kama bado upo hai usikubali kukata tamaa, usikubali kuishia njiani, sababu ya wewe kuwa hai mpaka sasa ni kuwa Mungu ana mpango na wewe. Ushindi mkuu upo mbele yako endelea kujaribu, endelea kujifunza kwenye makossa yako, endelea kutafuta watu ambao watakusaidia Zaidi.

Usisahau Kujiunga na MasterMind Coaching hapa >>>>https://goo.gl/gWbh7K

Nakutakia kila la Kheri

Rafiki Yako,

Jacob Mushi

Mwandishi na Kocha wa Mafanikio

www.jacobmushi.com/huduma

Andika Maoni Yako Hapa

Discover more from Jacob Mushi

Subscribe now to keep reading and get access to the full archive.

Continue reading