Siku Moja nilikuwa nawaza hivi, “Siku Nikifa Nikakuta hakuna Mungu Nitacheka Sana”, Sauti nyingine ndani yako Ikasema, “Hapo Utakapokuwa Unachekea ni Nani Huyo Atakuwa Amekutengenezea” Ndugu Yangu Mungu Yupo, Ukatae Ukubali…………………

Kuna ule mtazamo wa kuwaona watu ambao wamefanya mambo makubwa, na wale wenye ushawishi mkubwa sana kuwa hao ni watu wasio na makossa kabisa. Na hiyo hupelekea pale wanapokosea kitu cha kawaida kabisa mfano ndoa kuvunjika, tunawaona kama vile ni wamefanya makossa makubwa sana.

Wakati huo huo kuna watu wengi sana kila mara ndoa zao zimekuwa na matatizo makubwa na wanaishia kuachana bila hata kujulikana.

Rafiki napenda ufahamu kwamba kila mmoja ana jambo ambalo huwa ni udhaifu wake. Kila mmoja kuna kitu ambacho kimekuwa kinamshinda mara kwa mara hata wewe ukijitafakari utaona kunai le dhambi ambayo kila mara hukuangusha. Hata kama hakuna anaeijua basi wewe mwenyewe na Mungu wako ndio mnaijua vizuri.

Kama kwako kuna kitu kama hicho basi ina maana kwamba kila mtu kuna jambo ambalo limekuwa likimsumbua pia. Kila mmoja kuna ka udhaifu Fulani huwa kinamwangusha. Ndio maana katika wanafunzi 12 wa Yesu bado kulikuwa na mmoja Yuda Iskariote aliemsaliti Yesu kwa tamaa ya fedha. Bado pia kuna Petro ambaye alimkana Yesu mara tatu, kuna mwingine huyu anaitwa Thomaso alishindwa kabisa kuamini kama Yesu amefufuka mpaka amshike kwa mikono yake.

Sasa kama Yesu mwenyewe alijua amechagua watu 12 wazuri na bado wakaonekana wenye madhaifu mimi ni nani niseme sina dhambi hata kidogo? Ndio maana nataka kukwambia mimi ni mtenda dhambi kuliko wewe, Neema ya Mungu tu ndio hunisaidia, napenda ulijue hili ili usije kunihukumu siku moja ukisikia makosa niliyoyatenda. Vilevile hata wewe kuna kitu najua ni udhaifu wako, unakusumbua mara kwa mara, umekuwa unajaribu kuacha lakini unakwama.

Nataka uwe na mtazamo chanya kwenye mambo ya wengine uweze kuchukuliana na kila mtu kwasababu kila mmoja ana jambo ambalo linamsumbua sana ndani yake hata kama hatakwambia. Na haya mambo ndio mara zote huwaga ni siri za ndani ya watu.

Unaweza kuwa unasema sasa Jacob unataka kusema kila mmoja awe huru kufanya dhambi ile ambayo inamshinda? Hapana hapo utakuwa umenielewa vibaya, maana yangu hapa ni kuwa wewe utambue mtu akiwa hai na akakosea kwa chochote kile bado ana nafasi ya kutubu mbele za Mungu wake.

Inawezekana Mtu ametenda uovu ukasambaa sana akatubu kwa Mungu akapata msamaha na wewe ukaendelea kumhukumu, kumsema vibaya, kumuandika vibaya, ikatokea umekufa ukaenda kuhukumiwa kwa kutenda dhambi ya kuhukumu wengine. Maana yangu hapa kama wewe huna nafasi ya kwenda kumshauri au kumsaidia mtu aliekosea usipoteze muda wako kumsema na kumzungumzia kwasababu huenda unasema yule ni mtenda dhambi sana, kumbe alishatubu siku nyingi na kusamehewa.

Hakuna haja ya kuzungumza mabaya ya mtu kama huwezi kuzungumza mazuri yake. Hakuna haja ya kumchukia mtu alietenda maovu bali twapaswa kumuombea Mungu amsaidie. Na wewe binafsi ukishaujua udhaifu wako basi ni jukumu lako, kuhakikisha unakaa mbali na vile vitu ambavyo vinakupelekea kuitenda dhambi. Ukishatambua kile ambacho kinakuangusha kirahisi ni jukumu lako kutafuta msaada kwa watu wenye uwezo kwenye tatizo lako wakusaidie uweze kujidhibiti.

Rafiki Yako Jacob Mushi.

6 Responses

  1. Bro umezungumza fact Sana .
    Kuna watu wanatabia ya kuwajaribu watu wengine kwenye jambo fulani
    Lakini wasijue unaweza ukawa unajaribu mtu kumbe lile unalomjaribu ndio udhaifu wake
    Laiti wangelitambua hakuna aliyekamilika wasingehukumu kwa kuona umeshindwa katika hilo walilokujaribu
    Be blessed brother

Leave a Reply to Jacob MushiCancel reply

Discover more from Jacob Mushi

Subscribe now to keep reading and get access to the full archive.

Continue reading