Mtu Tajiri kuliko wote duniani kwa haraka haraka ukifikiria unaweza kudhani kilichomfanya akawa Tajiri ni pesa zake au akili zake pekee. Ila ukija kutafakari katika upande mwingine unagundua kwamba ukiwa na pesa pekee bila watu utaishia kuzitumia kwa matumizi yako binafsi. Ukiwa na akili nyingi za kugundua vitu halafu huna watu utaishia kugundua tu lakini uvigunduavyo haviwezi kufaidisha yeyote.

Nataka uanze kugundua kwamba akili zako, uwezo wako, pesa zako, nguvu zako zinategemea watu sana. Wenye utajiri mwingi umetokana na watu wengi waliowaamini na kuamua kufanya kazi pamoja nao. Embu jiulize kama watu tusingeamini Facebook, Mack asingekuwa bilionea leo. Ubilionea wake umetokana na watu kuamini kile anachokifanya.

Usianze kuwaacha watu nyuma yako ukafikiri unaweza kwenda mwenyewe. Pesa zako ili ziongezeke lazima uanze kuwafikiria watu. Ili zidumu Zaidi na kwa muda mrefu lazima uzipeleke kwenye kitu ambacho kinawasaidia watu. Kama ukipeleka pesa zako kwenye madawa ya kulevya zitapotea baada ya muda Fulani kwasababu hao wanunuaji wako hawataishi muda mrefu.

Chochote unachokifanya lengo lako kubwa liwe kuleta mabadiliko kwa wengine. Kama ambavyo wewe unavyoifurahia WhatsApp na kuendelea kuitumia ndio unasababisha mmiliki wake aendelee kuwa Tajiri. Sasa jiulize yeye angewaza kwenye kutengeneza pesa peke yake huenda tungeshaichoka hii WhatsApp.

Amazon inamuingizia pesa Jeff Bezos kwasababu kuna wateja wameiamini Amazon na wako tayari kuendelea kununua vitu kwenye mtandao huo. Vile vile kuna wauzaji ambao wameuamini mtandao na wakawa wanauza bidhaa zao. Embu jiulize amazon yenyewe bila watu pesa zinatengenezekaje?

Jiulize Mzee Bakhresa bila watu walioamini bidhaa zake za Azam angekuwa wapi? Angeishia kama wafanyabiashara wengine huku chini.

Ufanyeje?

Kila unachotaka kukifanya tazama kwa undani Zaidi watu wanakwenda kufaidikaje kuliko hata wewe. Unajua watu wkaifaidika ndio wataendelea kununua kila siku.

Tumia muda mwingi kujifunza juu ya watu na tabia zao.

Usianzishe jambo ili tu upate faida bali ili watu wapate faida.

Tengeneza watu wengi wanaokuamini kwasababu huo ndio uwekezaji mkubwa kuliko hata fedha. Ukiwa na watu elfu ambao wanakuamini unaweza kukopa pesa na ukafanya biashara bila wasiwasi.

Watu wanakuja kwako kwasababu ya matatizo yao na sio matatizo yako. Ni muhimu ukawa mtu unaejali matatizo ya watu kwasababu hapo ndipo panapoanzia kujenga uaminifu na kuaminiwa na wengi.

Chochote unachokifanya hakikisha kinaleta mabadiliko chanya kwenye Maisha ya wengine.

Nakutakia Kila la Kheri.

Rafiki Yako Jacob Mushi.

www.jacobmushi.com/huduma

4 Responses

Leave a Reply to Jacob MushiCancel reply

Discover more from Jacob Mushi

Subscribe now to keep reading and get access to the full archive.

Continue reading