“Vile nilivyojieleza kwako kuhusu mimi mara nyingi inaweza kuwa ni vile nilivyotaka wewe unifahamu mimi lakini inaweza kuwa mimi halisi sio huyo niliekuelezea.” Jacob Mushi
Tumekuwa tunapata muda wa kukaa na watu, muda wa kazi, muda wa kuperuzi na kujua yanayoendelea duniani lakini mara chache sana tumekuwa tunapata muda wa kukaa na sisi.
Kiwango unachojifahamu kinatokana na kiwango cha muda unaoutenga na kukaa na wewe. Unapopata utulivu sehemu peke yako unaweza kugundua mengi sana ambayo yapo ndani yako.
Ni vigumu sana kujua umefika wapi kimaendeleo ya ndani kama huna muda na wewe. Kuna mengi sana utashindwa kugundua namna ya kurekebisha kama hukai peke yako na kutafakari Maisha yako.
Kwa kupitia kufikiri ndipo vitu vingi vimegunduliwa. Bahati mbaya sana dunia ya sasa imekuwa ndio inaondoa utulivu wa watu kuliko kipindi kingine. Watu wanatumia muda mwingi Zaidi kuperuzi kuliko kukaa na kutulia wakitafakari Maisha yao jinsi yanavyokwenda.
Kama huna muda na wewe ni ngumu sana watu wengine kuwa na muda na wewe. Anza kwanza kuwa na muda na wewe.
Ubora wa Maisha yako ya ndani unatokana na namna unavyotenga muda wa kujitengeneza mwenyewe. Matatizo mengi ya nje yanasababishwa na namna tulivyo ndani na sio jinsi tulivyo nje.
Jipende, jisikilize, utagundua mengi sana yaliyojificha.
Tenga Nusu Saa kila siku kwa ajili ya Tafakari.

Rafiki Yako,

Jacob Mushi

Andika Maoni Yako Hapa

Discover more from Jacob Mushi

Subscribe now to keep reading and get access to the full archive.

Continue reading