Habari Rafiki Karibu kwenye blogu hii tujifunze pamoja mambo haya NILIYOJIFUNZA KUTOKA KWENYE KITABU. Mwandishi P. T. Barnum anazungumzia namna ya kutengeneza uchumi wetu binafsi na kufikia utajiri. Kwa kupitia yale maisha tunayoishi kila siku kuna mengi tunakosea bila kujua.

Kama dunia nzima ingekuwa haikuoni, au ungekuwa mwenyewe huku duniani, vitu ulivyonavyo sasa hivi ungeendelea kutamani kuwa navyo? Nguo unazopenda kuvaa ungeendelea kuvaa? Kama jibu ni hapana basi unaishi maisha kwa kufuata macho ya watu wanaokutazama kila siku. Na aina hiyo ya maisha ni magumu sana hutaweza kufikia ndoto zako. Utakuwa kila unachokifanya ni ili kuwaridhisha wale wanaokuangalia.
Tumekuwa tukijichimbia shimo la umaskini kila siku kwasababu ya kutaka kuwa na muonekano wa kitajiri kwa nje huku ukweli ukiwa ni hatuna huo utajiri tunaotaka kuuonesha kwa watu. Haina maana yeyote kuwaonesha watu kwamba na wewe una pesa wakati ndani unajua fika huna. Unachotakiwa kufanya ni kutumia muda huo wa kuwaonesha watu kutengeneza yale maisha unayotaka.
Ili uweze kuufikia utajiri na uhuru wa kifedha hakikisha kinachoingia siku zote ni kikuwa kuliko kinachotoka. Nikiwa namaanisha matumizi yawe madogo kuliko mapato. Hata kama mapato yataongezeka matumizi nayo yakue lakini si Zaidi ya mapato.
Maisha yanazidi kuwa magumu kwasababu ya vitu tunavyovipa vipaumbele kumbe havina umuhimu wowote kwenye maisha yetu.

Soma: Kitabu: Mbinu 101 za Mafanikio 

Wale wote unaotaka wajue kwamba wewe una pesa na una maisha mazuri, wakijua au wasipojua hakuna kitakachoongezeka kwenye maisha yako upande wa kifedha. Zaidi sana utakuwa unajiongezea mzigo mkubwa wa kutaka kuwaridhisha watu ambao hawajali chochote juu ya maisha yako. Na hapo ndipo utakuwa unaanza kuifuata njia ya umaskini mwenyewe.
Msingi wa maisha ya mafanikio na furaha ni afya njema. Kama huna afya njema huwezi kuishi maisha ya furaha vile vile huwezi kuzitafuta pesa kama inavyotakiwa. Ili uweze kutunza afya yako inapaswa kuzifuata sharia za asili ambazo zinatuongoza katika maisha. Kufanya mazoezi, kula vizuri (chakula bora) kutunza mazingira na mengine yote ya asili unayoyajua.
Ulevi wa pombe na sigara ni mojawapo ya mambo yatakayokufanya ushindwe kufanikiwa katika safari yako ya mafanikio. Unapokuwa mlevi huwezi hata siku moja kufanya maamuzi yenye akili. Akili yako inapokuwa imejazwa na athari za ulevi huwezi kuwa na matokeo bora. Kama mtu atakuwa na mafanikio akaanza tabia hizi basi ndio mwanzo wa kupotea njia au kuporomoka kabisa.

Kamwe usikope kwa ajili ya vitu vya kula au mavazi. Hata kama mtu atasema anakuamini kwa kiasi kikubwa uchukue tu uje kulipa siku nyingine usikubali. Unajibebesha mizigo ambayo itakuwa inakutesa.

Kufanyia kazi madeni ya vitu ambavyo ulishatumia kama nguo, au chakula mwandishi anasema ni sawa na kufanyia kazi farasi aliekufa maana yake hakuna matunda yeyote utakayopata kwa kile unachokifanyia kazi. Utajikuta kila pesa unayopata inakwenda kuishia kwenye madeni kwasababu ulikopa kwa ajili ya matumizi.
Karibu Sana.
Jiunge na Usiishie Njiani hapa…  http://jacobmushi.com/jiandikishe/
Jacob Mushi

#USIISHIE_NJIANI

Andika Maoni Yako Hapa

Discover more from Jacob Mushi

Subscribe now to keep reading and get access to the full archive.

Continue reading