Habari za Leo ni matumaini yangu u mzima na unaendelea vyema. Leo tuanajifunza nguzo 10 za mafanikio yako. Ukiweza kuzisimamia nguzo hizi lazima utaona mabadiliko na kusonga mbele kuelekea kwenye ndoto zako. Karibu tujifunze pamoja mpaka mwisho.
Jua kusudi la kuzaliwa kwako.
Nguzo ya kwanza na ya muhimu sana ni wewe kutambua kwanini ulizaliwa. Upo duniani kwa shughuli ipi. Ukishatambua upo duniani ili kufanya nini huu ndio msingi mkuu na utakupa mwelekeo wa maisha yako. Bila kutambua kusudi la kuwepo duniani maisha yako hayawezi kua na mwelekeo wowote na utajikuta unafanya chochote kinachokujia mbele yako. Ili uweze kuishi maisha yenye furaha ni pale utakapoweza kuligundua kusudi la wewe kuwepo duniani na kuanza kuliishi. Huwezi kuwaza hata siku moja kama upo sahihi au umepotea.
Tambua uwezo ulio nao.
Nguzo ya pili ukishatambua kwanini umezaliwa duniani, lazima pia ujue una uwezo wa aina gani na uutumieje ili kutimiza lile kusudi lako. Kila mmoja ana uwezo wa kipekee sana kutokana na kile alichozaliwa kuja kukifanya huku duniani. Aliezaliwa kuhubiri atakua anaongea sana bila kuchoka. Mwimbaji ataimba sana na atakua na sauti ya kipekee inayovutia. Mchezaji mpira atakua na uwezo wa aina yake katika kucheza mpira labda ni golikipa atadaka kwa uwezo wa kipekee, na mfunga magoli vile vile. Usipotambua uwezo wako hutaweza kuliishi kusudi na kufikia mafanikio makubwa. Usipojua Makali ya upanga yako wapi hutajua pa kunoa. Ni vyema sana ujue uwezo wako uko wapi ili uweze kufanyia mazoezi uwe bora kila siku.
Kua na ndoto kubwa za kutimiza kusudi.
Nguzo namba tatu ni uwe na ndoto kubwa. Usikubali kuishia kua wa kawaida tu. Tengeneza maono yako makubwa ya kuifikia dunia nzima. Maono na ndoto zako ndizo zitakazo kulinda wewe. Kama ni mwalimu basi kua na ndoto za kufundisha mataifa na mataifa na wengi wabadili maisha yao kupitia mafundisho yako. Ndoto kubwa zinakupa hamasa na nguvu Zaidi za kuendelea kusonga mbele. Kama huna ndoto kubwa ni rahisi sana kuja kuacha kufanya hicho unachokifanya. Ni rahisi sana kukata tamaa endapo huna picha kubwa ya kile uanchokifanya. Ndoto kubwa zinakupelekea wewe ujifunze na uweze kupata ujuzi mpya wa kukusaidia kuzitimiza. Hakikisha una ndoto kubwa.
Weka malengo.
Nguzo ya tano ni malengo. Malengo ndio njia au ramani ya wewe kufikia yale maono yako na ndoto zako. Malengo ndio kiongozi wako, malengo yanakuonyesha ni nini cha kufanya sasa na cha kufanya baadae. Malengo yanakuonyesha umepiga hatua gani hadi sasa au baada ya muda Fulani. Bila malengo haundi popote. Wanasema ukitaka kumla tembo unamgawanya vipande vipande. Hivyo ndoto zako kubwa unazigawanya vipande vipande ili uweze kuzitimiza. Lazima uwe na malengo ya muda mfupi na muda mrefu. Muda mfupi ni kuanzia malengo ya siku, wiki, mwezi miezi mitatu, mwaka, hadi miaka mitano. Malengo ya muda mrefu ni kuanzia miaka kumi, kumi na tano hadi ishirini. Weka malengo sasa katika sehemu zote za maisha yako. Kiroho, kifamilia, malengo binafsi (Ndoto zako), malengo ya kiuchumi, na mahusiano. Malengo ndio yanakuongoza
Fanyia kazi malengo yako.
Pamoja na kuweka malengo yote hayo hayawezi kutimiza usipoyafanyia kazi. Anza kufanyia kazi malengo yako kila siku kila mwezi na fanya tathmini ya kile unachokifanya angalia matokeo unayopata ili upate picha kama unasogea mbele au unarudi nyuma. Bila kufanyia kazi malengo hakuna muujiza utakaoweza kutokea na malengo yakatimia. Fanya kazi kwa bidii sana na utaona matokeo ya kazi zako. Hakuna aliepambana bila kukata tamaa na asione matokeo. Wakati mwingine usikate tamaa pale unapoona mambo ni magumu ongeza bidi na hakikisha umejua tatizo liko wapi na ulirekebishe. Mara nyingi tatizo linaweza kua wewe hujajifunza vizuri, au huna uwezo wa kutosha lakini hivyo vyote sio sababu ya kuacha songa mbele na rekebisha pale kwenye makosa ili uweze kupiga hatua kuelekea mbele kwenye ndoto zako.
Jifunze kila siku.
Katika safari yako utakutana na vikwazo na magumu mengi sana. Ni kwasababu unapita njia ambayo hujawahi kuipita. Hivyo unahitaji maarifa ndani ya akili yako ili uweze kufanikiwa. Kua na muda ambao umeutenga kwa ajili ya kujifunza na kukuza ufahamu wako juu ya kile unachokifanya. Kujifunza kila siku ni muhimu sana kwasababu mambo yanabadilika kila siku. Na watu hawaachi kufikiria njia mpya kila siku. Kama kuna mahali utakosea ni ukishindwa kuwekeza kwenye ubongo wako. Kuna vitu unajifunza leo vitakuja kukusaidia miaka mitano ijayo sio lazima unachojifunza leo kilete matokeo leo leo. Anza sasa hujachelewa soma vitabu, sikiliza cd, angalia video za mafundisho ujaze ubongo wako maarifa. Ipo siku utaona matunda ya unachokijaza kwenye ubongo wako.  Unachokiotesha sasa utakivuna siku moja.
Kua na Nidhamu.
Ili uweze kufikia mafanikio kila siku lazima ujijengee nidhamu ya kufanya mambo mbalimbali hasa katika yale malengo yako. Yako mengi sana katika nidhamu ya kuzingatia. Kama nidhamu ya kujifunza, nidhamu ya kuamka mapema, nidhamu ya fedha, nidhamu ya matumizi ya mitandao ya kijamii, nidhamu katika kutunza muda. Ukikosa nidhamu utajikuta unafanya mambo bila matokeo au kurudia rudia pale ulipo kila siku. Nidhamu ndio inayowaangusha wengi kuna wakati utakua unahitajika kufanya jambo Fulani lakini akili yako ikakwambia umechoka. Kama huna nidhamu utajikuta unaisikiliza akili yako. Ukiwa mtu wa nidhamu mafanikio yanakufuata popote unapokua maana bila nidhamu tutajikuta tunafanya mambo bila mpangilio na kupata matokeo ya hovyo.
Uadilifu.
Uadilifu ni kitu cha muhimu sana katika safari ya mafanikio. Lazima ujue ni vitu gani vya kujitenga navyo. Bila hivyo utajikuta unaanguka huko mbele. Sifa yako katika jamii ni ipi? Watu wanakutazama wewe kama mtu wa namna gani? Uvaaji wako unatafsiri yule mtu unaemsema? Matendo yako yanatoa picha gani? Marafiki ulionao mnafanana na manelekea safari moja? Haya ni maswali ya muhimu sana kujiuliza ili ujue uadilifu wako ukoje. Watu wanaokuzunguka wanapata picha gani kuhusu wewe. Kama picha waliyonayo sio ile unayoisema wewe na inatokana na matendo yako mabovu huwezi kufikia mafanikio. Kuna wakati wanaweza kua na picha ya zamani juu yako lakini ukweli ni wewe unao.
Uvumilivu na Imani
Uvumilivu ni nguzo ya muhimu katika mafanikio. Kuna wakati utafanya na hutaona matokeo. Kuna wakati utafanya na hutaona hata wa kukutia moyo. Kuna wakati utakutana na vikwazo na magumu mengi yanayokatisha tamaa uvumilivu unahitaji. Kwasababu umeshaona unachokipigania kuvumilia hadi ukipate ni juu yako. Hakuna wa kukuzuia ila ni wewe mwenyewe. Ukiamua leo kusema sifanyi tena ni wewe utakua umeacha sio waliosema hutafika mbali. Uvumilivu unaletwa na Imani yako juu ya kile unachokifanya. Kadiri Imani yako ilivyo kubwa na ndivyo unavyoweza kuvumilia kwa muda mrefu. Imani ni kua na uhakika wa mambo yasiyoonekana. Zile ndoto zako kubwa haziwezi kutimia kama hauna Imani na uvumilivu. Imani yako juu ya ndoto zako kubwa inajengwa na matendo yako ya kila siku kuziendea ndoto zako. Imani bila matendo imekufa. Ukiacha tu sisi tuanajua hukua unakiamini unachokifanya ulikua unabahatisha ulikua unajaribu.
Jiamini.
Jiamini kwenye kile unachokifanya usikubali nguvu ya nje ikushinde, usikubali maneno ya watu yakufanye uache kutimiza ndoto zako.
Maneno yana nguvu lakini hayazidi nguvu uliyonayo ya kuyakataa au kuyakubali.
Tumia nguvu uliyonayo kuyakataa maneno hasi yanayokupoteza katika kuitimiza ndoto yako. Ili uweze kuaminiwa unatakiwa ujiamini wewe kwanza. Uanze kuamini mwenyewe ndoto zako kabla wengine hawajaziamini. Uanze kuzikubali ndoto zako kabla wengine hawajazikubali au kuzikataa. Watu wengi tumekua na tabia ya kusikiliza sauti za nje kuliko sauti zetu wenyewe. Mtu yupo tayari kuacha kitu kwa kushawishiwa na marafiki zake au ndugu zake wa karibu. Unaonyesha ulivyo dhaifu kwa kukubali kusikiliza sauti za nje na kuacha kufanya kile roho yako inatamani kufanya.
Anza na kujiamini, ziamini ndoto zako kuliko mtu mwingine yeyote. Nakuhakikishia ushindi ni lazima.
Je umekua ukisuasua hujui ni kwanini upo duniani? Mpaka sasa hujatambua muelekeo wako wa maisha? Hujui ufanye nini?
Unatamani kujifunza lakini huna watu wakukuhamasisha kujifunza?  Bonyeza hapa www.jacobmushi.com/coach

Rafiki Yako,

Jacob Mushi

www.jacobmushi.com/coach

Andika Maoni Yako Hapa

Discover more from Jacob Mushi

Subscribe now to keep reading and get access to the full archive.

Continue reading